Tuesday 12 January 2016

MAPINDUZI DAY: KWANINI MAPINDUZI,KWANINI MUUNGANO na Majjid Mjengwa

Ndugu zangu,
Ningelipenda kuwa Zanzibar katika siku kama ya leo. Ningelipenda kuwa Zanzibar siku kama ya leo miaka 52 iliyopita.
Ndio, usiku wa kuamkia leo, miaka 52 iliyopita, yaani, Januari 12 , 1964, siku ya Jumapili, ndio ilikuwa Siku ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Mapinduzi ya Zanzibar ni sura ya kipekee katika kitabu cha historia ya Bara hili. Nimepata kuandika, kuwa kwetu sisi wa Bara, jambo la Zanzibar ni letu, imani hiyo pia iko visiwani, kuwa jambo la Bara ni lao.Tuko jirani mno na tuna historia ya pamoja. Ni ndugu wa damu.
Nimepata kuwa Zanzibar mara nyingi. Nimepata nafasi ya kuongea na WaZanzibar. Nimedadisi Mapinduzi yale ya 1964, nimedadisi Muungano wetu.
Na tujifunze kupitia historia. Nimeamini siku zote, kuwa historia ni Mwalimu Mzuri sana. Maana, hatuwezi kuyajua ya leo kama hatuyajui ya jana. Na hivyo, hatutoweza kupata mwanga kwa yatakayotokea kesho.
Shuleni nilipenda sana kusoma habari za Wanamapinduzi wa dunia hii. Kusoma habari za mapinduzi ya umma katika sehemu za dunia. Habari za Mapinduzi ya Zanzibar zilinivutia sana. Nilipata kusoma kitabu cha John Okello kilichonivutia sana kuhusu Mapinduzi ya Zanzibar. Kiliitwa ' Zanzibar Revolution'.
Kupitia historia hiyo nilifahamu habari za wanamapinduzi; ni watu wa aina ya Abdurahman Babu, Edington Kissasy, Kassim Hanga na wengineo. Nilipomaliza Form Four pale Tambaza Secondary nilifanya safari ya kwanza maishani mwangu kuvuka bahari. Safari ya kwenda Unguja.
Huko nilikuwapo wakati wa sherehe za Mapinduzi Januari 12, 1989. Ni wakati wa utawala wa Dr Salmin Amour. Nilifurahia kuwapo mahala palipokuwa na vuguvugu la Mapinduzi ya mwaka 1964. Kuviona kwa macho na kutembea kwenye vitongoji vya Zanzibar; Mkunazini, Ziwani, Fuoni, Mji Mkongwe na kwengineko.
Mwandishi Ryszard Kapuchinski alikuwapo Dar es Salaam na Zanzibar wakati wa mapinduzi. Kapuchinski anaandika; kuwa Karume alikuwa Dar es Salaam wakati mapinduzi yale yakiendelea kule visiwani. Kapuchinski anamzungumzia Karume kama mtu aliyekuwa akiongea kwa sauti ya juu sana hata ukikaa nae karibu. Mara nyingi Karume alikuwapo pale New Africa Hotel, mahali walipokutana wanamapinduzi wengi wa bara hili.
Ninapotafakari mitazamo tofauti juu ya dhana ya Mapinduzi ya Zanzibar, na kwa vile nimepata bahati ya kufika visiwani na kuongea na WaZazibar na wa Mji Mkongwe na wa mashambani, kuna uhalisia ninaouona, kuwa suala la Zanzibar na hususan Muungano si jepesi kama wengine wanavyofikiri, au wanavyotutaka tufikiri.
Maana, Muungano ni zao la Mapinduzi ya 1964. Yale ya 1964 yalikuwa ni Mapinduzi ya Umma. Ni Mapinduzi ya Wajamaa wa Kiafrika. Ni muhimu watu wakajua historia sahihi ya Mapinduzi, lakini, yumkini swali muhimu leo si nani aliyewaongoza wakulima, wavuvi na wakwezi wale kufanya mapinduzi, bali, kuyafahamu malengo ya mapinduzi yale na kama yamefikiwa.
Naamini, kuwa kuuvunja Muungano leo ni kuvunja misingi ya uwepo wa Tanganyika kama dola. Kuna hasara kidogo sana kubaki kwenye muungano, na hasara na madhara makubwa zaidi kuwa nje ya Muungano.
Zanzibar ya jana, leo na kesho, itabaki kuwa ni mkusanyiko wa wenyeji wa asili mbali mbali. Na wengi ni Waafrika wa kutokea Tanganyika. Mathalan, Zanzibar ina WaZanzibar wenye asili ya Unyamwezi, Usukuma, Umakonde, Uluguru, Uzaramo, Undengereko, Urabau, Ushiraz na kadhalika. Hivyo basi, swali gumu ni je, Mzanzibar ni nani nje ya Muungano? Unafikiri haya unapokutana na Wazanzibar wenye kuongea Kinyamwezi lakini hawajawahi kukanyaga Sikonge wala Urambo, Tabora.
Bila shaka, Mwalimu Nyerere aliposema kama ingewezekana Zanzibar isogezwe na upepo iwe mbali na Tanganyika huenda ingekuwa nafuu, naye alikuwa akisumbuliwa na ukweli huo. Kuwa ni vigumu kwa Tanganyika kuondokana na Zanzibar katika uhalisia uliopo. Tulivyo sasa, suala la Zanzibar ni letu Tanganyika, na la Tanganyika ni la Zanzibar pia.
Yalikuwa malengo sahihi, ya waasisi wa Muungano kuwa uanze na Serikali MBILI kwa lengo la kwenda kwenye Serikali MOJA. Na kuunganisha vyama; Afro Shiraz na TANU ulikuwa ni mwanzo wa safari ya kuelekea kwenye kuyafikia malengo hayo. Maana, Serikali kibaraka wa Sultan iliyopinduliwa 1964 haikuwa na malengo ya kuukomboa umma wa Zanzibar ulio na mchanganyiko wa hata wenye asili ya Bara. Serikali iliyoundwa na ZNP na ZPPP ilikuwa ni mabaki ya Usultani ambao wanyonge walio wengi visiwani hawakuwa na faida nao.
Huu ni wakati wa kujitafakari. Ni wakati wa kujisahihisha pia. Kuyaacha malengo ya waasisi ya kuufikia Muungano Kamili wa Serikali MOJA kutoka kwenye Serikali MBILI, na kubadili mwelekeo kwenda kwenye Serikali TATU, kimsingi itakuwa ni kuianza safari ya kurudi Tanganyika na Zanzibar pasipo MUUNGANO.
Zanzibar inatokaje kwenye mkwamo huu wa kisiasa?
Tumesema, historia ni mwalimu mzuri. Itakumbukwa, kuwa baada ya matokeo ya uchaguzi wa mwaka 2005 Maalim Seif alikaririwa akitamka kuwa; 'Hakuna tena mufaka wa tatu". Rais Karume naye akakaririwa akitamka; "Sitaki kusikia habari ya Serikali ya mseto".
Hakuna namna nyingine ya Zanzibar kutoka kwenye mkwamo huu bila pande mbili kukaa kwenye meza ya mazungumzo na kuafikiana katika kuwapa wananchi kufanya uchaguzi wa wanachokitaka. Pande zote mbili kwa namna moja au nyingine zimecheza rafu kwenye uchaguzi uliopita.
Uchaguzi mpya ukisimamiwa na wenye kuaminiwa na pande mbili utaivusha Zanzibar salama. Ni wakati sasa wa pande mbili kuamua kusonga mbele kwa kuzika chuki zao kwenye kaburi la sahau.
Tunaona, hata kwa mgogoro uliopita, kwa njia ya mazungumzo, CUF na CCM Zanzibar walifikia muafaka, na Serikali ya Mseto ikapatikana. Na mara hii tena tunaamini muafaka utafikiwa na Serikali ya Mseto itaendelea kuwepo, hakuna namna nyingine ya kuviongoza visiwa vya Zanzibar bila mseto.
Kuna umuhimu pia wa viongozi wa CCM na CUF kufahamu kuwa dunia imebadilika. Leo dunia inafuatilia kwa karibu yanayotokea kwetu kwa vile yana mahusiano na athari hata nje ya mipaka yetu. Sura ya dunia imekuwa ikibadilika katika vipindi tofauti. Marekani, kwa sababu za kimaslahi imekuwa na historia ya kuingilia mambo ya ndani ya sio tu nchi za kiafrika, hata nchi za Marekani ya Kusini, Asia na hata Ulaya.
Katika karne hii, tukubaliane, kuwa hakuna tena masuala ya ndani ya Tanzania , Zimbabwe, Uganda au Ushelisheli. Dunia imebadilika. Yanayotokea Mji Mkongwe Unguja na Micheweni Pemba yanaihusu Idara ya Ulinzi ya Marekani, Pentagon, Shirika lake la ujasusi CIA na hata FBI. Tuiangalie dunia ya sasa kwa miwani hiyo.
Itakumbukwa baada ya Vita Kuu ya Pili, dunia ilipitia kipindi cha vita baridi . Miaka ile ya 60 dunia iligawanyika katika kambi mbili kubwa kiitikadi; zilijulikana kama Warsaw Pact na Nato Pact. Kambi ya Warsaw iliongozwa na Urusi ya zamani na ile ya NATO iliongozwa na Marekani. Kulikuwepo pia na kundi la nchi zisizofungamana na upande wowote. Tanzania ilikuwa mwanachama wa kundi hili. Hata hivyo, nyingi ya nchi hizi kimsingi zilikuwa na upande zilizoegemea kati ya makundi mawili niliyoyataja.
Tunasoma kuwa Marekani na hususan kupitia Shirika lake la ujasusi la CIA ilijiingiza kwa mara ya kwanza katika siasa za Zanzibar mara baada ya mapinduzi ya 1964 kwa lengo la kupunguza kasi ya kuenea kwa Ukomunisti. Marekani iliingiwa na hofu ya Zanzibar kama kisiwa kutumiwa na Wakomunisti. Katika Zanzibar bado kuna kumbukumbu ya historia hii kwa kuyaangalia majina kama Uwanja wa Mao Tse Tung, hospital ya V.I Lenin, shule za Fidel Castro, Patrick Lumumba na mengineyo. Yote haya yalikuwa na mwelekeo wa kambi ya Warsaw; Ukomunisti.
Mvutano wa kiitikadi kati ya Warsaw na NATO uliendelea kuwepo hadi pale ukuta wa Berlin uliopoangushwa Agosti 23, 1989. Huo ndio ulikuwa mwisho wa vita baridi ya dunia. Marekani ikabaki bila mpinzani wa kiitikadi. Kuanzia hapo upepo wa kisiasa uligeuka ghafla, wimbi la demokrasia ya vyama vingi likaanzia Ulaya Mashariki na kuikumba Afrika.
Kati ya mwaka 1990 hadi 1998 tulishuhudia kuwepo kwa ombwe la kiitikadi. Uchaguzi wa Zanzibar wa mwaka 1995 ulifanyika kukiwa na ombwe hilo la kiitikadi duniani. Miaka mitatu baadae, Agosti 7, 1998, sura ya dunia ilianza kubadilika. Ni mara ile balozi za Marekani Nairobi na Dar Es Salaam zilipolipuliwa. Septemba 11, 2001 sura ya dunia ilibadilika ghafla, pale kikundi cha kigaidi cha Alqaida kilipofanya maangamizi makubwa katika miji ya Washington na New York. Hii ni tafakuri endelevu..
Happy Mapinduzi Day!
Maggid Mjengwa,
Dar es Salaam.(P.T)

No comments:

Post a Comment

Maoni yako