Sunday 15 March 2015

"MSIOZESHE WATOTO WENU WAKIWA WANAFUNZI" Mama Salma Kikwete asisitiza

Wazazi na walezi wilayani Mafia wametakiwa kutokubali kupokea mahari za watoto wao wakiwa wanafunzi bali wawasimamie na kuhakikisha wanasoma kwa bidii na kufika elimu ya chuo kikuu.

Rai hiyo imetolewa jana na Mke wa Rais Mama Salma Kikwete wakati akiongea na wanafunzi pamoja na wazazi wa shule ya Sekondari Bweni iliyopo kata ya Kanga wilaya ya Mafia mkoani Pwani.

Mama Kikwete ambaye ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) alisema baadhi ya wazazi wanapokea mahari za watoto wao na kuwaozesha wakiwa na umri mdogo jambo ambalo huwafanya kukatisha masomo yao na wanawanyima haki yao ya msingi ya kupata elimu.

"Mtoto akisoma atakuwa na maisha mazuri hapo baadaye ataweza kufanya kazi za kitaalamu za kuajiriwa au kujiajiri yeye mwenyewe, kujikomboa na umaskini, kuwasaidia wazazi wake, ataepukana na mimba za utotoni na kujiepusha na maradhi yanayotokana na ngono zembe kwani elimu ni msingi wa kila kitu".
Mke wa Rais Mama Salma Kikwete akiongea na wananchi wa Kijiji cha Bweni katika Kata ya Kanga waliofika shuleni hapo kwa ajili ya kusalimiana naye.

No comments:

Post a Comment

Maoni yako