Wednesday 2 September 2015

Mhe.TUNDU LISSU AMJIBU DR.SLAA

Sikiliza sauti ya Mhe.Tundu Lissu akihojiwa

Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Wilbroad Slaa, jana alitangaza rasmi kuachana na siasa baada ya kutofautiana na chama chake katika kumpokea Edward Lowassa na hatimaye kumfanya mgombea urais wa chama hicho chini ya mwamvuli wa UKAWA.

Dr. Slaa alitoa uamuzi huo jana mbele ya waandishi wa habari ambapo pia mbali na kutangaza kuachana na siasa aliwatuhumu Lowassa na Sumaye kuwa ni MAFISADI wa kutupwa na kwamba hawastahili kupewa nchi .

Akijibu tuhuma za Dk. Slaa mwansheria wa CHADEMA Tundu Lissu amesema anashangaa kwamba Dr. Slaa anadai hakubaliani na uteuzi wa Lowassa kwa ajili ya kiti cha rais wakati yeye ndiye aliyepanga na kumleta Lowassa katika chama hicho.

Lissu amesema kinachomsumbua Slaa ni tamaa ya Urais maana CHADEMA walikuwa wamekwisha mteua kugombea urais tangu mwezi mwezi wa kwanza.

"Kamati kuu ilimteua kugombea urais kwa tiketi ya chadema tangu mwezi january na ilipofika mwezi April kamati ilimthibitisha tena kuwa yeye ndo mgombea wetu.

"Ilipofika mwezi wa tano, Dr. Slaa mwenyewe akaanzisha mazungumzo ya kumleta Lowassa Chadema.

"Amesema mshenga ni Gwajima,hajasema mposaji ni nani. Nani aliyemfuata Gwajima kumwambia tunamtaka Lowassa, ni Dr. Slaa mwenyewe.

"Yeye ndiye aliyemwambia Gwajima halafu ndo akamwambia Mwenyekiti wa chama kuwa Lowassa akikatwa tumchukue, na tumchukue kwa sababu ana nguvu kubwa na ataipasua CCM katikati.

"Mbowe alipoambiwa hivyo alikubali na Dr. Slaa ndiye aliyeunda timu ya majadiliano ya Chadema yenye wajumbe watatu ambao ni Benson Kigaila, John Mrema, Reginald Munishi.

"Walikaaa na kufanya mazungumzo ya kina na Dr. Slaa alishiriki kila hatua.Majadiliano hayo yalikamilika tarehe 22.7.2015 ambapo Slaa aliitisha kikao cha kamati kuu cha dharura chenye ajenda moja tu ya kumkaribisha Lowassa ili awe mgombea urais wa Chadema." Amesema Lissu

Kwa nini Dr. Slaa amewasaliti?
Tundu Lissu amesema kilichomfanya Dr. Slaa awageuke ni First Lady, kwa maana ya mke wake ambaye hakukubaliana na kitendo cha Slaa kumpisha Lowassa

Lissu amedai kuwa wakati Lowassa anapokelewa tarehe 27 July kwenye Kamati Kuu, Dr.Slaa hakulala nyumbani, aliporudi nyumbani mchumba wake alimtupia mabegi nje na DR. alilala kwenye gari.

"Aliporudi nyumbani, Slaa alitupiwa mabegi nje, akalaa kwenye gari. Kesho yake akaja na kusema anataka kujiuzulu." Amesema Lissu na kuongeza:

"Slaa anasema hana chama na hajihusishi na chama chochote, lakini cha ajabu ni kwamba mwezi huu amepokea mshahara wa katibu mkuu wa chama, bado anatembea na gari ya katibu mkuu wa chama.

"Japokuwa amekitukana chama, lakini bado anatembea na magari ya chama, nyumba anayokaa alinunuliwa na chama na inalindwa na walinzi wa chama.

".....Ajitokeze atuambie ni nani aliyemwandalia huu mkutano wa serena hoteli? hizo gharama zimelipwa na nani? na kwa nini ametamka leo?

"....Kwa kuwa Slaa amekitukana chama, litakuwa ni jambo la busara sana kama atarudisha mali zote za chama."

Akizungumzia tuhuma zilizotolewa na Dr.Slaa dhidi ya Lowasaa, Lissu amesema CHADEMA walimhoji Lowassa kuhusu sakata la Richmond na aliwaambia kuwa aliyeruhusu mkataba wa Richmond uendelee ni Rais Kikwete
(Habari,picha na sauti kwa hisani ya Mpekuzi Blog)

No comments:

Post a Comment

Maoni yako