Wednesday 24 August 2016

WAPI TUNAELEKEA?: ASKARI POLISI WAUAWA NA MAJAMBAZI WAKIWA KATIKA LINDO CRDB BANK MBAGALA

Jeshi la Polisi limethibitisha kuwa jumla ya askari wake wanne wameuawa usiku wa kuamkia leo baada ya majambazi kuvamia tawi la benki ya CRDB lililopo Mbande, wilayani Temeke, Dar es Salaam.

Akizungumza moja kwa moja kupitia kituo cha Redio One Stereo leo asubuhi, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Simon Sirro, amesema watu kadhaa wamekamatawa na msako unaendelea ili kuwapata waliotekeleza unyama huo. Sirro amesema taarifa kutoka eneo la tukio zinaonesha kuwa majambazi hao walikuwa 14 na baada ya kufanya mauaji hao, walivamia kituo cha polisi cha Mbande kisha wakavunja stoo na kuchukua sare ya askari na silaha.

Akielezea namna tukio hilo lilivyotokea, Kamanda Sirro amesema wahalifu hao walitumia mwanya wakati askari wakibadilishana lindo katika taasisi hiyo ya fedha na kuibuka ghafla na kuanza kurusha risasi. Kwa mujibu wa Sirro, gari la polisi limechakazwa kwa risasi na askari mmoja aliyekuwa lindo alifanikiwa kukimbia na ndiye aliyeweza kutoa taarifa na maelezo ya namna tukio lilivyofanyika.

“Watu kadhaa wamekamatwa na tunaendelea na msako. Tunawataka wakiwa hai au wafu,” amesema Kamanda Sirro huku akiwataka watu kujihadhari na yeyote anayejitambulisha kwao kuwa ni askari bila kuonesha kitambulisho.

Ameendelea kusema kuwa baada ya operesheni ya kukomesha mtandao wa wahalifu kama hao na wengine kukimbilia nchi jirani, masalia wameanza kujikusanya na kutekeleza matukio ya mauaji huku askari wakiwa ndio walengwa.
Aidha CP Mssanzya aliwataja askari waliouawa katika tukio hilo wakati wakibadilishana lindo kuwa ni E.5761 CPL Yahya, F.4660 CPL Hatibu, G 9524 PC Tito na G 9996 PC Gastoni na raia wawili waliojeruhiwa aliowataja kuwa Ali Chiponda na Azizi Yahya wote wakiwa wakazi wa Mbande.

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe.Mwigulu Nchemba alifika katika eneo lilikofanyika tukio hilo na kumjulia hali Raia aliyejeruhiwa

No comments:

Post a Comment

Maoni yako