Monday 8 August 2016

CHADEMA NA POLISI NGANGARI HUKO CHALINZE

Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani limefuta mkutano wa hadhara wa Chadema uliopangwa kufanyika katika Uwanja wa Miembe Saba mjini Chalinze.

Mkutano huo uliokuwa ufanyike jana, ulikuwa uhutubiwe na Waziri Mkuu mstaafu na mjumbe wa kamati ya Chadema, Frederick Sumaye.

Mwenyekiti wa Chadema, Mkoa wa Pwani Baraka Mwago alisema jana kuwa alishangazwa na hatua hiyo ya ghafla ya polisi kwa kuwa mkutano huo ulifuata taratibu zote na Mkuu wa Polisi Wilaya ya Chalinze, aliruhusu kufanyika kuanzia saa 6.00 mchana hadi saa 12.00 jioni.

Alisema wakati maandalizi yote yakiwa tayari, ilipotimia saa nane mchana waliitwa polisi na kuelezwa kuwa mkutano huo umezuia kwa maelezo kuwa intelijensia ya polisi imeonyesha kuwa ungehudhuriwa na viongozi wengi wa kitaifa, hivyo polisi Chalinze haijajipanga kutoa ulinzi kwa viongozi hao.

“Hii sababu imetushangaza kwa sababu kiongozi wa kitaifa ambaye angehudhuria ni Sumaye peke yake."

Kwa mujibu wa Katiba ya Chadema kipengele cha 7.5.3 (f) inamtambua mjumbe wa kamati kuu au baraza kuu anayeishi katika mkoa kuwa ni mjumbe wa baraza la mkoa husika.

“Kutokana na kipengele hicho, Sumaye ana sifa za kuhudhuria mkutano huu kwa sababu anaishi Kiluvya wilayani Kisarawe,” alisema Mwagu.

Alisema lengo la mkutano huo, lilikuwa ni kuutambulisha uongozi mpya wa Chadema kwa wananchi baada ya kufanyika uchaguzi mdogo Juni 4, mwaka huu wilayani Mkuranga.

Katibu wa Chadema mkoani humo, Halfani Milambo alisema waliandika barua kuwataarifu polisi na likakubali, lakini walishangazwa kuzuiwa baada ya kufika katika Uwanja wa Miembe Saba walikotakiwa kufanya mkutano.

“Tuliwaandikia barua tarehe Agosti 4 na siku iliyofuata Agosti 5 tulikubaliwa na Mkuu wa Polisi Chalinze (OCD), SSP J. Magomi kufanya mkutano kwa masharti,” alisema.

No comments:

Post a Comment

Maoni yako