Thursday 14 July 2016

WALIOSEMA HAWAIVI CHUNGU KIMOJA? (Mhe Msigwa na Mhe Naibu Spika Tulia)

Jana katika ugawaji wa Madawati, waheshimiwa hawa walijikuta wakikaa meza moja na hata kupiga picha ya pamoja. Siasa pembeni katika kuwatumikia Watanzania

Rais Magufuli aliwapongeza Mbunge wa Iringa (Chadema), Peter Msigwa na Naibu Spika wa Bunge, Dk. Ackson Tulia, kwa kukaa pamoja katika meza kuu wakati wa hafla hiyo.

Wabunge kutoka vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) walitangaza kususia vikao vya bunge vinavyoongozwa na Dk. Ackson au shughuli yoyote itakayoongozwa naye kwa madai amekuwa akiendesha vikao vya bunge kwa upendeleo na kutaka avuliwe wadhifa huo.

Rais Magufuli alisema inapofika masuala ya kuleta maendeleo ya taifa, viongozi wanapaswa kuweka kando masuala ya vyama.

Alisema hata yeye wakati akipiga kampeni za uchaguzi mkuu mwaka jana, aliwaahidi Watanzania kuwa atawatumikia wote bila ya kuangalia vyama, kabila, dini wala rangi.

“Mmeacha vyama vyenu pembeni, mnaunga mkono maendeleo, leo unapomwona Msigwa na Tulia wapo jirani inatia moyo, ndicho tunachokitaka, nchi hii ni yetu sote, tukifanya hivyo nchi yetu itakuwa ya mfano,” alisema Rais Magufuli.

Alipoulizwa kwa kitendo chake cha kuhudhuria shughuli hiyo na kukaa meza moja na Dk, Ackson, Msigwa alisema wamefika katika hafla kama wajumbe wa Tume ya Utumishi ya Bunge.

Alisema pia walihudhuria hafla hiyo kwa sababu ni suala la maendeleo na walipaswa kushiriki ili kuhakikisha fedha hizo zinatumika kama zilivyopangwa.

“Hii shughuli haiendeshwi wala kuandaliwa na Tulia, ni shughuli iliyoendeshwa na tume yetu na ndiyo maana tupo hapa,” alisema Msigwa

No comments:

Post a Comment

Maoni yako