Friday 14 August 2015

MHE. WAZIRI MEMBE AKUBALI YAISHE

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, amefunguka kwa mara ya kwanza na kuweka wazi kilichotokea mjini Dodoma na kusababisha ashindwe katika uteuzi wa kuwania urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Membe amekuwa kada wa tatu kueleza hadharani jinsi uteuzi huo ulivyoendeshwa ambao Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli, aliibuka kidedea kati ya makada 42 waliojitokeza kuchukua fomu ya kuomba kuteuliwa.

Makada wengine waliojitokeza hadharani kuelezea mchakato huo ni Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalum), Prof. Mark Mwandosya, ambao kwa nyakati tofauti walieleza sababu mbalimbali zilizosababisha kushindwa kwao.
Membe akizungumza jijini Dar es Salaam jana katika kongamano la pili la Watanzania waishio ughaibuni (Diaspora), alisema mchakato huo ulikuwa ni sawa na timu mbili za mpira wa miguu zilizokuwa zinapambana uwanjani.
Alisema unaweza ukapata timu nzuri sana ya mpira kwenye ligi na ikashinda michezo yote bila kufungwa goli hata moja.
Aliongeza kuwa lakini mwishoni timu hiyo inapotoka sare na timu nyingine ambayo ni dhaifu kwenye fainali, timu hizo zinakwenda kwenye penalti kwa kuwa mshindi lazima apatikane.
Membe alieleza kuwa wakati wa upigaji penalti timu hiyo ambayo ilitarajiwa kuibuka na ushindi kwa kuwa ilicheza mpira safi ikafungwa penalti zote tano na hiyo timu ambayo haikutegemewa ikashinda mabao yote.
Alisema kuwa kwenye ‘football jargon’ kitendo hicho cha timu iliyocheza mpira vizuri na kudhaniwa ingeibuka na ushindi, lakini ikashindwa kwenye penalti, timu hiyo imekufa kifo cha ghafla.
Membe aliendelea kueleza kuwa timu hiyo itakuwa imepigwa kifo cha ghafla na kueleza kuwa inapopigwa kifo cha namna hiyo timu hiyo haiwezi kutegemewa isimame na ielezee kilichotokea.
“Naomba leo nitumie nafasi hii kwa mara ya kwanza kuelezea kilichotokea mjini Dodoma katika uchaguzi wa nafasi ya urais kwa Chama Cha Mapinduzi na nadhani sitaulizwa tena,” alisema Membe.
Mfano huo huenda ukahusishwa na wanachama wa CCM waliokuwa wanamuunga mkono Membe kama timu iliyokuwa inatumainiwa ingeshinda mchakato huo, huku Dk. Magufuli akielezwa kama timu ambayo haikudhaniwa kushinda kinyang’anyiro hicho kutokana na kutokuwa na makundi yaliyokuwa yanamuunga mkono.
Membe alikuwa na kundi kubwa la wafuasi akimfuatia Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa.
Lowassa na Membe walikuwa miongoni mwa makada sita ambao walipewa adhabu ya kufungiwa mwaka mmoja kuanzia Februari, mwaka jana hadi Mei, mwaka huu, baada ya kubainika kuwa walianza kampeni mapema kabla ya wakati kinyume cha kanuni za chama hicho.

No comments:

Post a Comment

Maoni yako