Thursday 8 December 2016

MHE,RAIS MAGUFULI AFANYA MABADILIKO YA VIONGOZI MBALIMBALI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 07 Desemba, 2016 amefanya uteuzi wa Katibu Mkuu mmoja na Mkuu wa Mkoa mmoja na pia amefanya mabadiliko madogo katika Wizara na Mikoa kama ifuatavyo;

Dkt. Magufuli amemteua Prof. Faustin Kamuzora kuwa Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais.Kabla ya uteuzi huo, Prof. Kamuzora alikuwa Katibu Mkuu Mawasiliano.

Rais Magufuli amemteua Mhandisi Mathew Mtigumwe kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Uvuvi na Mifugo anayeshughulikia Kilimo. Mhandisi Mathew Mtigumwe anachukua nafasi ya Dkt. Frolence Turuka ambaye ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.

Kabla ya uteuzi huo Dkt. Frolence Turuka alikuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi aliyekuwa akishughulikia Kilimo. Anachukua nafasi iliyoachwa wazi na Mhe. Job Masima ambaye ameteuliwa kuwa Balozi.

Rais Magufuli amemteua Dkt. Maria Sasabo kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano na atakuwa akishughulikia Mawasiliano. Dkt. Maria Sasabo anachukua nafasi iliyoachwa wazi na Prof. Faustin Kamuzora ambaye ameteuliwa Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais.

Pia Rais Magufuli amemteua Mhandisi Angelina Madete kuwa Naibu Katibu Mkuu Katika Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Mhandisi Angelina Madete anachukua nafasi iliyoachwa wazi na Dkt. Maria Sasabo aliyeteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano anayeshughulikia Mawasiliano.

Aidha, Rais Magufuli amemteua Dkt. Aloyce K. Nzuki kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii.

Wakati huo huo, Rais Magufuli amemteua Bw. Christopher Ole Sendeka kuwa Mkuu wa Mkoa wa Njombe.Bw. Christopher Ole Sendeka anachukua nafasi ya Dkt. Rehema Nchimbi ambaye amehamishwa kituo cha kazi na kuwa Mkuu wa Mkoa wa Singida.

Dkt. Rehema Nchimbi anajaza nafasi iliyoachwa na Mhandisi Mathew Mtigumwe ambaye ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Uvuvi na Mifugo anayeshughulikia Kilimo.

Katika hatua nyingine, Rais Magufuli amemteua Dkt. Osward J. Mashindano kuwa Msajili wa Hazina.

Dkt. Osward J. Mashindano anachukuwa nafasi ya Bw. Lawrence Mafuru ambaye atapangiwa kazi nyingine

Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasilino ya Rais, IKULU
Dar es Salaam

07 Desemba, 2016
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiongoza Kikao cha Baraza la Mawaziri kilichofanyika leo tarehe 07 Desemba Ikulu jijini Dar es Salaam. Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan pamoja na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa. PICHA NA IKULU

No comments:

Post a Comment

Maoni yako