Sunday 1 January 2017

MHE RAIS MAGUFULI ASEMA BEI YA UMEME HAITAPANDA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amewahakikishia Watanzania kuwa licha ya Mamlaka ya udhibiti wa huduma za Nishati, Maji na Mafuta (EWURA) kuridhia ombi la TANESCO la kupandisha bei ya umeme kuanzia Januari mosi,2017 bei ya umeme haitapanda.

Rais Dkt. Magufuli amezungumza hayo leo Jumapili ya Januari Mosi, 2016 wakati wa Ibada katika Kanisa la Bikira Maria Mama Mwenye Huruma,Kanisa Kuu Jimbo Katoliki la Bukoba anapoanza rasmi ziara ya kikazi ya siku mbili Mkoani Kagera.

Rais Magufuli ameshangazwa na kitendo cha watendaji waliopandisha bei ya umeme bila hata ya kushauriana na yeye, Makamu wa Rais,Waziri Mkuu au Waziri mwenye dhamana ya Nishati na Madini Prof Sospeter Muhongo na hivyo kumshukuru Waziri Muhongo kwa kutengua maamuzi hayo.

''Ninamshukuru sana Waziri wa Nishati na Madini kwa maamuzi ya kusitisha hayo kwa hiyo umeme hakuna kupanda bei,haiwezekani unapanga mikakati ya kujenga viwanda na hasa katika mikakati mikubwa ya nchi ya kusambaza umeme mpaka vijijini,na umeme huu unaenda kwa watu masikini walioumbwa kwa mfano wa Mungu halafu mtu pekee kwa sababu ya cheo chake anapandisha bei,hili haliwezekani'' Alisema Rais Dkt. Magufuli.'

Aidha, Rais Dkt Magufuli ameendelea kuwataka watanzania katika mwaka huu mpya 2017 kuendelea kufanya kazi kwa bidii kama maandiko matakatifu yanavyoelekeza kuwa asiyefanya kazi na asile badala ya kulalamika kuwa fedha zimepotea.

Kwa upande wake,Askofu Msaidizi Jimbo Katoliki la Bukoba,Askofu Methodius Kilaini,akitoa mahubiri kwa waumini waliohudhuria ibada hiyo amempongeza Rais Dkt Magufuli kwa uongozi wake imara,huku akisema kupungua kwa urasimu katika ofisi za umma kunatokana na utendaji kuongezeka na kuwataka wana Kagera na Watanzania kwa ujumla kumuunga mkono Rais Magufuli kwa kufanya kazi kwa bidii na uaminifu.
Mara baada ya Ibada ya Misa Takatifu iliyoongozwa na Askofu wa Jimbo Katoliki la Bukoba,Askofu Desderius Rwoma,Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli aliwatakia heri ya mwaka mpya waumini wa kanisa hilo na watanzania kwa ujumla.

Jaffar Haniu
Naibu Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Kagera.
01 Januari, 2017

No comments:

Post a Comment

Maoni yako