Tuesday, 7 June 2016

TUME YA TAIFA YA UCHAGUZI NEC: WAMETUMIA NA KINGINE WAMESAZA WAMKABIDHI RAIS MAGUFULI

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imekabidhi shilingi Bilioni 12 kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, zilizobaki baada ya uchaguzi mkuu wa Madiwani, Wabunge na Rais uliofanyika tarehe 25 Oktoba, 2015.

Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Jaji Mstaafu Damian Lubuva amekabidhi hundi ya kiasi hicho cha fedha kwa Rais Magufuli leo tarehe 07 Juni, 2016 Ikulu Jijini Dar es Salaam na kueleza kuwa bakaa ya fedha hizo haikuathiri kwa namna yoyote uchaguzi mkuu wa mwaka jana.

"Mheshimiwa Rais fedha ambazo tunakukabidhi, tulijibanabana sana, japo muda wenyewe ulikuwa mfupi lakini tulijibanabana sana bila kuathiri utendaji wa shughuli za uchaguzi, isije ikawa inatoa sura kwamba iliathiri, haikuathiri, na katika hali hiyo kama ambavyo wengi ni mashahidi, hatujisifii, lakini uchaguzi ulienda vizuri" Amesema Jaji Mstaafu Lubuva.

Akizungumza baada ya kupokea mfano wa hundi hiyo, Rais Dkt. John Pombe Magufuli ameipongeza Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa kuokoa fedha hizo na kuzirejesha serikalini ili zipangiwe majukumu mengine na ametaka taasisi nyingine za serikali ziige mfano huo wa uzalendo na kutanguliza maslahi ya taifa.

"Kitendo hiki ambacho mmekionesha leo, kinaonesha ni kwa namna gani Tume ya Taifa ya Uchaguzi chini ya uongozi wako Mheshimiwa Mwenyekiti ilivyo na watu makini na waadilifu sana, kwa sababu hizi fedha ambazo kwa lugha uliyotumia ni bakaa, kutokana na zile ambazo mlipewa zaidi ya Shilingi Bilioni 270, mkatumia shilingi Bilioni 261.6, mkabakiza shilingi Bilioni 12, mngeweza kuamua kusema hamkubakiza na hakuna mtu yeyote ambaye angewauliza, na saa nyingine pengine hakuna mtu yeyote ambaye angejua, mngeweza pia kusema kiasi mlichotupa hakijatosha, tunaomba mtuongezee ama mngetengeneza maneno mazuri mazuri ya matumizi, bado nina uhakika serikalini wasingejua" Amesema Rais Magufuli.

Pamoja na kukabidhi hundi ya bakaa ya shilingi Bilioni 12, Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Jaji Mstaafu Damian Lubuva amemuomba Rais Magufuli aisaidie tume hiyo kupata jengo lake la ofisi kwa kuwa hivi sasa tume inatumia majengo ya kupanga ambayo yanaigharimu tume hiyo takribani shilingi Bilioni 1 na Milioni 400 kila mwaka kwa kulipia kodi ya pango, usafiri na gharama nyingine za uendeshaji.

Rais Dkt. John Pombe Magufuli amelikubali ombi hilo na kuamua kuwa fedha ambazo Tume ya Taifa ya Uchaguzi imeziokoa (Shilingi Bilioni 12) kutoka kwenye Uchaguzi Mkuu wa Mwaka jana zitumike kujenga ofisi ya tume, na amependekeza ofisi hiyo ijengwe mkoani Dodoma.

"Na mimi ningefurahi zaidi kama hilo jengo lingejengwa Dodoma, kwa sababu Dodoma ndio makao makuu ya nchi hii, na hasa kwa sababu Dodoma ni katikati ya Tanzania" Amesisitiza Rais Magufuli.

Rais Magufuli pia amelikubali pendekezo la tume hiyo la kuanzishwa kwa mfuko wa tume ya uchaguzi ambao utakuwa unakusanya fedha kila mwaka kwa ajili ya uchaguzi mkuu unaofuata, badala ya kuendelea na utaratibu wa sasa wa kusubiri mwaka wa uchaguzi ndipo zitengwe fedha zote za kugharamia uchaguzi huo.

Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
Dar es Salaam

07 Juni, 2016

MASANJA MKANDAMIZAJI ASEMA "KARIBU TULE"

Monday, 6 June 2016

NAWATAKIA MFUNGO MWEMA WA RAMADHANI

BAADA YA MAUAJI YA KIKATILI MWANZA NA TANGA; VIKOSI VYAINGIA MASKANI KUSAKA WAHALIFU

Watu watatu wanaosadikiwa kuwa majambazi,wameuawa katika majibizano ya risasi na askari polisi mkoani Mwanza,alfajiri ya kuamkia jana jumapili katika mapango ya mlima wa Utemini yaliyopo kata ya Mkolani jijini Mwanza.
SERIKALI imetuma kikosi maalumu cha ulinzi, kikiongozwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kwa ajili ya kuwasaka watu wanaodaiwa kuwa majambazi ambao wanaendesha mauaji ya kinyama mkoani Tanga.

"HILO NALO NENO"

DIAMOND PLATNUMZ ACHANGIA MADAWATI 600 JIJINI DAR ES SALAAM

Kundi la WCB Wasafi wakiongozwa na Rais wa kundi hilo, Mwanamuziki Diamond Platnumz wakiwasili katika ofisi za Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda kwa ajili ya tukio hilo la kutoa machango wa wa Madawati 600 kwa Mkoa wa Dar.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe. Paul Makonda akimpongeza Mkurugenzi wa WCB, msanii Naseeb Abdul 'Diamond Platinumz' mara baada ya kumtembelea ofisini kwake na kutoa mchango wake wa madawati yapatayo 600 kwa ajili ya kuchangia maendelea ya mkoa.

Akiongea katika makabidhiano hayo msanii huyo alisema ni jambo jema kwao kuweza kujitolea mchango huo ili kuweza kumuunga mkono Mhe. Makonda katika kukabilana na changamoto za elimu.

Sunday, 5 June 2016

KATUNI YA LEO

RAIS MAGUFULI AHUDHURIA IBADA KANISA LA MZEE WA UPAKO

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza jambo wakati akiagana na Mchungaji Anthony Lusekelo‘Mzee wa Upako’ katika kanisa lake la Maombezi lililopo Ubungo Kibangu jijini Dar es Salaam. Rais Dkt. Magufuli alihudhuria ibada hiyo pamoja na kukagua barabara inayotoka Ubungo Kibangu hadi Barabara ya Mandela eneo la Riverside.

Saturday, 4 June 2016

MAENDELEO YA MAKAZI AFRIKA; NIGERIA KUJENGA DUBAI YAO JIJINI ABUJA

Naibu Waziri wa Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Angelina Mabula yupo nchini Nigeria kuhudhuria kikao cha Mkutano Mkuu wa 35 wa Shelter Afrique Jijini Abuja. Tanzania imechaguliwa kuwa mwenyeji wa Mkutano wa 37 utakaofanyika nchini Tanzania mwaka 2018.
Mchoro huu juu na chini unaonyesha taswira ya mji wa kisasa unaotabiriwa kuwa Dubai ya Nigeria unaojengwa nje kidogo ya Jiji la Abuja ujulikanao kama Centenary City Abuja ambao wajumbe wa nchi mbalimbali za Afrika waliohudhuria Mkutano Mkuu wa 35 wa Shirika la Makazi Afrika waliweza kuutembelea na kujionea ndoto ambayo wanigeria wameamua kuitekeleza.

R.I.P MOHAMMED ALI

Usiku wa kuamkia leo ulimwengu umefikiwa na habari za kifo cha mwanamasumbwi mahiri kupata kutokea hapa duniani, ni Muhammad Ali.
Muhammad Ali, atakumbukwa kama shujaa wa wanyonge wa dunia. Alikuwa bondia na mwanaharakati wa haki za wanyonge. Daima Ali hakukubali kuburuzwa.